Tangazo

Pages

Wednesday, May 23, 2012

ONESMO NGOWI KUONGOZA UJUMBE MZITO WA MASUMBWI DUNIANI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
 
Rais wa Shirikisho la Ngumi la Kimataifa katika bara la Afrika (IBF) Onesmo Ngowi wa Tanzania ataongoza ujumbe mzito toka  Afrika na Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi katika mkutano wa 29 wa Shirikisho la Ngumi la Kimataifa na Chama Cha Ngumi Cha Marekani (IBF/USBA). Mkutano huo utafanyika katika jiji la Honolulu, kwenye jimbo la Hawaii nchini Marekani alikozaliwa Rais wa sasa wa Marekani Barak Obama.
 
Jimbo la Hawaii linajulikana sana duniani kama jiji la starehe ambalo hupokea watalii wengi sana duniani wanaokwenda kule kustarehe. Hawaii ni jimbo lililoko Kaskazini mwa nchi ya Marekani likiwa karibu zaidi na bara la Asia!
 
Ujumbe wa Afrika na Mashariki ya Kati atakaoungoza Ngowi utajumuisha viongozi na wanachama wa Shirikisho la IBF katika nchi za Afrika ya Kusini, Botswana, Namibia, Uganda, Ghana, Cote D’Ivoire, Morocco,  Tunisia, Dubai, Oman na Jordan.
 
Hii ni mara ya kwanza kwa Onesmo Ngowi kuongoza ujumbe toka Afrika na Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi kwani mara zote huwa anaongoza ujumbe wa bara la Afrika katika mikutano ya IBF/USBA. Kuongezewa wigo wa madaraka kwa Ngowi kumekuja wakati ambapo IBF/USBA inapanua wigo wa shughuli zake katika masoko yanayoinukia hususan katika mataifa yanayozalisha mafuta kwa wingi duniani.
 
Mashariki ya Kati ni moja na sehemu zenye utajiri mkubwa sana duniani kutokana na uzalishaji wake mkubwa wa mafuta na gesi. Nchi ya Dubai ambayo ni kiungo kikubwa sana cha biashara za kimataifa ikiziunganisha Ulaya, Asia na mataifa mengine ya Marekani, Afrika imeteuliwa na IBF kuwa ni kitovu cha shughuli zake Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi.
 
Baadhi ya wajumbe mashughuri watakaokuwa katika msafara huo na nchi zao kwenye mabano ni pamoja na: Issac Tshabalala, Alfred Bugwane, Branco Milenkovic (Afrika ya Kusini), Justin Juuko (Uganda), John Akaba (Cote D’Ivoire), Skeikh Ahmed Omar (Morocco), Mohammed Hatimy (Tunisia) Sheikh Khalifa Hassan, Mohammed Othman (Dubai), Yakub Yossef (Jordan), Julian Homaulaba (Botswana), Michael Tetteh, Henry Mann-Spain (Ghana) na Hussein Mohammed (Oman).
 
Katika mkutano huo unaotarajiwa kuanza May 29 mpaka Juni 2, Ngowi atawasilisha rasimu ya mradi wa IBF wa Utalii wa Michezo (IBF Sports Tourism) katika kikao hicho baada ya kuteuliwa na mkutano wa mwaka jana uliofanyika katika jiji la Las Vegas, liliko kwenye jimbo la Nevada nchini Marekani. Katika kikao cha mwaka jana Ngowi alitakiwa kuja na rasimu ya mradi wa IBF wa Utalii wa Michezo ambapo nchi za Tanzania na Ghana ziliteuliwa kama nchi za majaribio katika bara la Afrika.
 
Kufanikiwa kwa mradi huu kutaifanya Afrika hususan Tanzania kufaidi sana kutokana na mtandao mpana wa IBF ambao uko katika nchi zaidi ya 203 duniani. Katika mradi huu IBF wa Utalii wa Michezo wanachama wa IBF katika nchi hizi watashawishiwa kuzitembelea Tanzania na Ghana kama watalii pamoja na kuwekeza katika miradi mbalimbali.
 
Aidha katika mradi huu IBF itafanya mikutano yake ya robo mwaka na mwaka katika nchi za Tanzania na Ghana ikikuza utalii. Mikutano ya mwaka ya IBF/USBSA huudhuriwa na watu zaidi ya 3000 toka nchi zaidi ya 203 kila mwaka.
 
Imetolewa na,
 
Kitengo cha Mahusiano (PRO)
International Boxing Federation Africa (IBF/Africa)
 
Benjamin William Mkapa Pension Towers
Mezzanine Floor,
Dar-Es-Salaam - Tanzania
 
Technology House, 35-38 Ghalla Road
P.O BOX 1106 MOSHI - TANZANIA
Tel/Fax: 255-27-2754743

No comments:

Post a Comment