Tangazo

Pages

Friday, August 26, 2016

ULINGO Briggs alimduwaza Klitschko


ILIKUWA ni ndani ya ukumbi wa Hamburg, nchini Ujerumani usiku wa kuamkia Oktoba 16,2010 pambano la kikatili lilipofanyika kwa kuwakutanisha ndani ya ulingo bingwa wa WBC, Vitali Klitschko raia wa Ukraine aishiye Ujerumani dhidi ya Shannon Briggs wa Marekani.
Utangulizi
Lilikuwa ni pambano la raundi 12, ambapo katika raundi zote hizo, pambano lilikuwa likipiganwa kinyama bila huruma likiwa ni pambano la kuwania ubngwa WBC uzani wa juu, huku Klitschko akitetea ubingwa wake kwa ushindi wa pointi.
Raia huyo wa Ukraine pamoja na kutawala pambano hilo kwa raundi zote akirusha ngumi nzito zilizotua kichwani kwa Mmarekani huyo, lakini alishindwa kabisa kumkalisha chini kwa makonde.
“Nimeshangazwa sana namna alivyostahimili, nilimchapa makonde mengi mazito na nimemchana lakini hakuanguka hata kidogo, Briggs anastahili sifa,”anaeleza Klitschko baada ya pambano hilo.
Katika pambano hilo, majaji wote walitoa alama 120-107, 120-107 na  120-105 kwa  Klitschko, ambaye kwa ushindi huo alijiwekea rekodi ya kushinda mapambano 41 akipigwa 2 wakati  Briggs alivurunda rekodi yake na kuwa 51-6-1.
“Nimepigana na George Foreman, nimepigana na Lennox Lewis, lakini Vitali ni zaidi, alinipiga ngumi nzito sana ana kasi ya ajabu katika mikono yake, kwangu mimi hili ni pambano bora,” anaeleza Briggs baada ya pambano hilo
Pambano ndani ya ulingo
Klitschko katika pambano hilo alikuwa akitumia ‘jab’ za kushoto kumwinda Briggs kisha akawa anamaliza na  ngumi kali ya kulia yaani ‘big right’. Ndiivyo alivyoanza hivyo pambano hilo, alikuwa akimtupia jab ndani ya dakika mbili za raundi ya kwanza kisha kuvurumisha konde kali la mkono wa kulia.
Kabla Briggs hajakaa sawa, akapigwa ‘left hooks’ mbili kidevuni kisha M-Ukraine huyo akaachia fataki jingine la mkono wa kulia, Briggs akawa anajaribu kujibu mashambulizi bila mfanikio.
Klitschko alikuwa akipiga ‘kombinesheni’ katika raundi ya tatu lakini Briggs akawa anatumia ngumi za hesabu yaani ‘counter-punches’.
Klitschko alipiga ‘right hook’ safi mwishoni mwa raundi hiyo ya tatu na akaendelea kutoa adhabu katika raundi ya nne.
Raundi ya tano, Briggs alijikakamua na kupiga ngumi kadhaa huku akiendelea kupokea kipigo kikali kutoka kwa Klitschko.
Katika raundi ya 10, Briggs aligeuzwa kuwa begi la mazoezi ya ngumi na Klitschko alikuwa akichagua pa kupiga lakini alimshitukiza Klitschko alipoachia ngumi kali ya kulia  katika raundi ya 11, lakini Klitschko akaibuka kwa ngumi mbili kali za kulia zilizofanya  kichwa cha Briggs kuvimba kwa nyuma.
Lakini Briggs alishika kichwa na kugoma kabisa kupigwa KO na kuendelea na pambano na hadi mwisho Klitschko akaambulia ushindi wa pointi.
Shannon Briggs aliwahi kupigwa na George Foreman kabla ya kudundwa na Lennox Lewis mwaka 1998.
**Mwandishi ni kocha wa mchezo wa ngumi anayefundisha klabu mbalimbali Dar es Salaam. Anapatikana kwa simu 0713/0787- 406938 au email: superdboxingcoach@gmail.com

No comments:

Post a Comment