Tangazo

Pages

Tuesday, August 23, 2016

JIFUNZE MASUMBWI NA SUPER D COACH

ULINGO..
 
Ngumi ya Chavez yakatisha uhai wa Johnson
Na Rajabu Mhamila

LEO katika safu yetu ya fahamu ulingo nitabadili aina ya mfululizo wa makala zangu kwa kuwaandikia mashabiki makala kuhusiana na moja ya athari za mchezo huu.
 
Nitazungumzia ngumi iliyopigwa katika raundi  11 ya pambano kati ya  Leavander Johnson wa Marekani mkazi wa Atlanta  dhidi ya Jesus Chavez wa Mexico.

Pambano hilo lilikuwa ni la kuwania taji lake la Shirikisho la Kimataifa la Ngumi za Kulipwa (IBF), ambapo Johnson alikuwa bingwa na alikuwa akitetea ubingwa wake dhidi ya raia huyo wa Mexico.

Pambano lilifanyika usiku wa Jumamosi ya Septemba, 2005 kwenye ukumbi wa  MGM Grand Hotel- Casino, Las Vegas Nevada huko Marekani.

Kwa hakika ilikuwa ni pambano kali, kumbuka walikuwa wakipigana katika uzito wa lightweight yaani uzito mwepesi, na walikuwa wakijibizana makonde na kufanya pambano hilo kuwa na msisimko mkubwa

Leavander Johnson alikuwa ameahidi mashabiki wake wakiwemo wazazi wake waliofika ukumbini kushuhudia pambano hilo kuwa angetetea vema ubingwa wake na kwamba angemgalagaza mpinzani wake.

Kumbuka kwamba kocha wake alikuwa ni baba yake mzazi huku meneja wake akiwa ni kaka yake. Ukumbini pia walikuwepo mama yake mzazi na ndugu zake wegine ambao waliishuhudia ngumi iliyowaachia majonzi

Kuanzia raundi ya kwanza Leavander Johnson alionekana kama angeweza kuibuka shujaa kwani alikuwa akirusha makonde yaliotua kichwani kwa mpinzani wake na umati ukawa ukishangilia kwa nguvu

Hata hivyo kufikia raundi ya tano, mambo yakaanza kubadilika, Jesus Chavez ambaye  alikuwa kana kwamba anausoma mchezo wa mpinzani wake, akaanza kujibu masambulizi kwa makombora ya nguvu na kufanya pambano kuwa gumu na lisilotabirika kirahisi.

Johnson, aliyekuwa akitokea Jiji la Atlantic  N.J. alikuwa amepigana karibu miaka 16 hadi alipopata ubingwa huo wa dunia katika uzito wa ratili 135 sawa na karibu kilo 58 na alitwaa taji hilo mwezi  Juni 2005 na sasa alikuwa akitetea ubingwa wake kwa mara ya kwanza.

Raundi ya sita, saba nane hadi kumi hazikuwa na mabadiliko makubwa sana kwa aina ya mchezo wao kwani pambano lilikuwa ni piga nikupige, lakini hata hivyo  Jesus Chavez ambaye ni mzoefu, alionekana kutawala pambano kwa muda mrefu kwa kumpiga ngumi nyingi mpinzani wake.

Ndipo ilipoingia raundi ya 11. Kengele ililia kuashiria kuendelea na pambano katika raundi hiyo, Chavez akipigana kwa  kujiamini zaidi alitoka kwenye kona yake na kumvaa moja kwa moja Johnson aliyekuwa bado na ulevi wa  makonde ya raundi ya kwanza.

Mwanzoni tu mwa raundi hiyo, Johnson akarusha jab yake, lakini ikapishana na ngumi  ya kulia ya Jesus Chavez, Johnson akapigwa ngumi ya kushoto na kumfanya ayumbe huku akiwa ameweka mikono yake yote usoni kujikinga na adhabu zaidi.

Jesus hakutaka kuiacha nafasi hiyo, akavurumisha ‘combination’ mfululizo kwa Johnsona na ngumi nyingi zikampata kichwani, wakati mwamuzi wa pambano hilo anaingilia kati kumwokoa Johnson, ngumi kali ya kulia ya Jesus ikatua kichwani kwa Johnson na kumfanya atake kuanguka,  ndipo mwamuzi alipofika na kusimamisha pambano.

Johnson akawa amepoteza ubingwa wake kwa Chavez, mwamuzi katikati ya ulingo akawashika mikono wote wawili kisha kunyanyua mkono wa Chavez na kumtangaza mshindi kwa Technical KnockOut (TKO).

Hata hivyo, Johnson alidondoka kwenye chumba cha kuvalia nguo na kukimbizwa haraka  Kituo cha Afya cha Chuo Kikuu na kufanyiwa upasuaji wa ubongo uliochukua muda wa dakika 40 kujaribu kuokoa maisha yake .

Alibaki akiwa hana fahamu kwa wiki nzima akiwa anapumulia mashine,  lakini baadaye akaanza kupata nafuu jambo lililowapa matumaini ndugu zake waliokuwa wameshakumbwa na hofu ya 'kuondokewa' na ndugu yao mpendwa.

Akiwa anaelekea kupata nafuu, ghafla  hali yake ikabadilika na kuwa mbaya. Hali ilikuwa mbaya zaidi na ndugu zake wakashikwa na uchungu kuona ndugu yao akiteseka na maumivu ya kupumua kwa mashine, wakaamua kuiondoa na  maisha ya Johnson  yakakoma milele.

"Hatukuwa na njia zaidi ya kumsaidia asife, kwa hiyo ndugu zake walikuwa sahihi kuamua kuondoa mashine ya kupumulia," alisema Dk. William Smith aliyemfanyia upasuaji

Promota wa Johnson  Lou DiBella  alisema:” familia ya  Johnson ilikuwepo wakati akikata roho, baba yake ambaye alikuwa kocha wake, kaka yake aliyekuwa meneja wake na mama yake walikuwepo, jambo ninaloweza kusema ni kwamba  amekufa akiwa bingwa, amefia mchezo alioupenda:” alisema " DiBella.
*
**Mwandishi ni kocha wa mchezo wa ngumi anayefundisha klabu mbalimbali Dar es Salaam. Anapatikana kwa simu 0713/0787- 406938 au email: superdboxingcoach@gmail.com

No comments:

Post a Comment